MAGONJWA
 yasiyoambukiza yanachangia  kwa kiasi kikubwa katika kupunguza kasi ya 
maendeleo yetu kwani gharama za matibabu yake ni kubwa mno, si kwa kaya 
zinazoathirika tu bali kwa Taifa zima. 
Lishe
 duni pamoja na ulaji usiofaa na mitindo ya maisha vinachangia kwa kiasi
 kikubwa katika ongezeko la magonjwa yasiyo ya kuambukiza hususan kwa 
vijana na watu wazima; ambao ndiyo nguvu kazi kwa Taifa letu. 
Kauli
 hiyo ilitolewa hivi karibuni na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa  wakati 
akifungua mkutano wa tano wa wadau wa masuala ya lishe,  jijini Dodoma. 
Alisema ni muhimu wadau hao kuweka mikakati kupunguza kasi ya ongezeko 
la magonjwa sugu yasiyo ya kuambukiza. 
Waziri
 Mkuu alisema magonjwa hayo yanapaswa kudhibitiwa kwa kuzingatia ulaji 
unaofaa na mtindo bora wa maisha. Ni jambo lisilopingika kuwa hatua za 
kukabiliana na magonjwa ya kusendeka (mfano matatizo ya moyo, saratani, 
kisukari na shinikizo kubwa la damu), zinapaswa kuchukuliwa.
Alisisitiza
 dhamira ya Serikali ya Awamu ya Tano, inayoongozwa na Rais Dkt. John 
Magufuli ni kujenga uchumi wa viwanda ambao utatuwezesha kufikia uchumi 
wa kati ifikapo mwaka 2025, hivyo ni muhimu suala la lishe bora likapewa
 kipaumbele.  
Alisema
 kauli mbiu ya mkutano huo “Kuelekea Uchumi wa Viwanda: Lishe Bora ni 
Msingi wa Kuendeleza Nguvu Kazi yenye Tija” inatoa hisia chanya ya 
kufikia azma hiyo kwa kuwa maendeleo ya Taifa yanategemea sana uwepo wa 
nguvu kazi ya kutosha na madhubuti.  
Alifafanua
 kuwa miongoni mwa matatizo ya lishe duni ni pamoja na upungufu mkubwa 
wa vitamini na madini kwa watoto walio chini ya umri wa miaka mitano 
(5), wanawake walio katika umri wa kuzaa na wajawazito, vijana balehe 
pamoja na wakina baba. 
Waziri
 Mkuu alisema kuwa ni dhahiri kuwa tunahitaji kuanzisha viwanda 
vitakavyozalisha vyakula vilivyoongezwa virutubishi muhimu ili 
kurahisisha upatikanaji wa vyakula hivyo katika jamii zetu.  
“Nitoe
 wito kwa wadau wote hususan sekta binafsi kutumia fursa zilizopo na 
kuwekeza katika viwanda vya usindikaji wa vyakula vinavyozingatia 
viwango vya ubora. Niwahakikishie kuwa Serikali imeandaa mazingira 
mazuri ya uwekezaji, kwa hiyo, tumieni kikamilifu nafasi hiyo.” alisema 
Waziri Mkuu, Majaliwa 
Alisema
 kwa pamoja, wanaweza kuimarisha mikakati yao ya kuivusha nchi na watu 
wake kutoka katika lindi la umaskini na kujenga nguvu kazi imara 
itakayoweza kuhimili changamoto za maendeleo ya viwanda.  
Waziri
 Mkuu anatumia fursa hiyo kutoa rai kwa wadau wote, waendelee kuiunga 
mkono Serikali kwa kuwekeza katika utekelezaji wa sera na mikakati 
mbalimbali ambayo inalenga kuboresha hali ya chakula na lishe miongoni 
mwa jamii, hususan kwa watoto, wanawake walio katika umri wa kuzaa, 
vijana balehe na watu wenye mahitaji maalum kilishe. 
“Kwa
 msingi huo, Serikali imejumuisha masuala ya lishe katika Mpango wake 
Jumuishi wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka Mitano (2016/2017 – 2020/2021), 
kama eneo la kipaumbele katika kuboresha na kuendeleza nguvu kazi ya 
Taifa.” 
Waziri
 Mkuu aliongeza kuwa “dhamira ya Serikali ni kutokomeza aina zote za 
utapiamlo kwa kuwekeza na kuweka mazingira wezeshi kwa wadau wote 
kushiriki katika kuchangia utekelezaji wa afua za lishe nchini ambazo 
zina matokeo ya haraka miongoni mwa makundi yote yanayoathirika.” 
Alisema
 jitihada hizo zinalenga kutimiza azma ya Baraza la Umoja wa Mataifa la 
“Muongo wa Kuchukua Hatua katika Masuala ya Lishe – Decade of Action on 
Nutrition” ya mwaka 2016 hadi 2025 na pia kuwezesha kufikiwa kwa Malengo
 yote 17 ya Umoja wa Mataifa ya Maendeleo Endelevu (United Nations 
Sustainable Development Goals).  
Alibainisha
 kuwa Serikali inaendelea kutilia mkazo suala la uhamasishaji miongoni 
mwa watunga sera na viongozi katika ngazi mbalimbali kuhusu masuala yote
 yanayohusiana na lishe kwa lengo la kuwa na uelewa wa pamoja kuhusu 
masuala hayo.  
Alisema
 juhudi hizo zinaenda sambamba na utoaji wa elimu sahihi ya lishe kwa 
umma kwani tunaamini kuwa Watanzania wakielimishwa vizuri kuhusu masuala
 haya itachangia kuleta mabadiliko chanya katika jamii pamoja na taasisi
 zetu kwa ujumla.  
Alisema
 Serikali imeendelea kuongeza rasilimali kila mwaka kwa ajili ya 
kutekeleza masuala ya lishe hususan katika ngazi za mikoa na 
halmashauri, ambapo takwimu zinaonesha kuwepo kwa ongezeko kutoka 
wastani wa sh. milioni 65 mwaka 2011/2012 hadi kufikia sh. milioni 219 
mwaka 2016/2017.  
Kwa
 mwaka 2017/2018 Serikali ilikadiria kutumia jumla ya sh. billioni 11 
katika utekelezaji wa masuala ya lishe katika ngazi ya halmashauri, 
hivyo hadi kufikia robo ya tatu ya mwaka 2017/2018, kiasi cha sh. 
bilioni mbili zilitolewa na kutumika.  
Kadhalika,
 Waziri Mkuu aliendelea kuhimiza kuhusu suala la kutenga kiasi cha 
shilingi 1,000 kwa idadi ya watoto wenye umri wa chini ya miaka mitano 
katika Halmashauri zetu kupitia mapato ya ndani ili ziweze kutumika 
katika kutekeleza Afua hizo kwenye Halmashauri husika.  
Aliwahakikishia
 wadau hao kuwa, Serikali itaendelea kutenga fedha kwa ajili ya 
kugharamia utekelezaji wa Afua za Lishe kama zilivyoainishwa katika 
Mpango wa Taifa wa Utekelezaji wa Masuala ya Lishe 2016/2017 – 
2020/2021; kwa kadiri hali itakavyoruhusu. 
“Nitoe
 rai kwa Watendaji Wakuu wote katika Wizara husika, Idara, Wakala na 
Taasisi za Serikali, wadau wa maendeleo, asasi za kijamii; kila mmoja 
kwa nafasi yake au mamlaka yake, kuendelea kutenga fedha kwa ajili ya 
utekelezaji wa Mpango wa Taifa wa Utekelezaji wa Masuala ya Lishe.”  
Alisema
 mikoa na halmashauri zihakikishe kuwa afua zilizoainishwa katika mpango
 huo zinajumuishwa katika mipango na bajeti zao za kila mwaka, sambamba 
na kutoa fedha zilizopangwa kwa ajili ya utekelezaji.  
Waziri
 Mkuu alisisitiza tena kuwa kila mdau anayeshiriki katika utekelezaji wa
 shughuli za lishe nchini aoneshe bayana mchango wake katika kukabiliana
 na utapiamlo nchini ili Taifa liweze kufikia malengo tuliyojiwekea. 
Alisema
 ili wahakikishe hatua tunazochokua katika mapambano dhidi ya utapiamlo 
zinaleta matokeo kama walivyopanga na zinawanufaisha au zinawafikia 
walengwa, aliwaagiza  viongozi wa Serikali katika ngazi mbalimbali 
kutambua wajibu wao na kushiriki kikamilifu katika kudhibiti na 
kukabiliana na athari za utapiamlo katika maeneo yao. 
Pia,
 Waziri Mkuu aliwataka viongozi hao wa Serikali katika ngazi za 
mbalimbali wafanye tathmini ya ufanisi wa hatua wanazochukua na watoe 
taarifa za ufanisi au changamoto mara kwa mara.  
Kwa
 upande wake,Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Kazi, 
Vijana, Ajira na Walemavu, Jenista Mhagama  alisema ushirikishwaji wa 
wadau kwenye masuala ya lishe umeongezeka na wanashuhudia wadau wengi wa
 maendeleo wakionesha nia na wengine kuwekeza katika masuala ya lishe 
nchini. 
 Aidha,
 Waziri Jenista alisema wameweza kuratibu wa uanzishwaji wa mabaraza 
mbalimbali yanayojadili masuala ya lishe likiwemo baraza la sekta 
binafsi ambao wana mchango mkubwa katika kuhakikisha azma ya Serikali ya
 kutokomeza utapiamlo inafikiwa.  
Alisema
 hatua hizo kwa kiasi kikubwa zimechangia kupunguza viwango vya 
utapiamlo pamoja na idadi ya vifo kwa watoto wenye umri chini ya miaka 
mitano. “Mfano mzuri ni pale tulipopunguza udumavu kutoka asilimia 42 
mwaka 2010 hadi asilimia 34.4 mwaka 2016.” 
Alisema
 Taifa linahitaji nguvu kazi imara itakayohimili ushindani katika soko 
la ajira na kuendeleza Tanzania ya Viwanda. Nguvu kazi hiyo inaanza 
kujengwa kwa kuimarisha lishe bora hususan kuanzia pale mama anapokuwa 
mjamzito hadi mtoto anapofika miaka miwili.  
Awali,Waziri
 wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu, 
alisema viwango vya matatizo ya lishe vimepungua kwa baadhi ya viashiria
 ingawa si kwa kiasi cha kuridhisha. 
Alitaja
 moja ya viashiria vya kupungua kwa matatizo ya lishe ni kushuka kwa 
tatizo la udumavu, ambapo kwa sasa kuna wastani wa watoto watatu wenye 
udumavu kati ya watoto 10 walio katika umri chini ya miaka mitano.
Waziri
 Ummy alisema kuwa udumavu huathiri ukuaji wa mtoto kimwili na kiakili, 
hivyo kupunguza uwezo wa kufanya vizuri shuleni na kupunguza ufanisi 
wake katika maisha yake ya utu uzima.
Alitaja
 mikoa ambayo imeathiriwa zaidi na tatizo hilo la lishe ni pamoja na 
Rukwa, Njombe, Ruvuma, Iringa, Kagera, Mwanza na Geita, ambayo ina 
wastani wa zaidi ya asilimia 40. Mikoa hiyo ni kati ya mikoa yenye 
uzalishaji mkubwa wa chakula nchini.
“Ni
 dhahiri kuwa, utatuzi wa suala hili unahitaji mbinu na hatua za haraka 
pamoja na ushirikiano wa kila mmoja wetu. Kulingana na takwimu za 
kidemografia na afya ya mwaka 2015/2016, watoto 106,000 wana utapiamlo 
mkali ukilinganisha na watoto 340,000 wenye utapiamlo wa kadiri.” 
Alisema
 idadi hiyo inaashiria kuwa watoto hao wenye utapiamlo mkali wapo kwenye
 hatari kubwa ya kupoteza maisha, ambapo hadi sasa changamoto kubwa 
waliyonayo ipo katika utambuzi wa tatizo, utoaji wa rufaa, upatikanaji 
wa chakula dawa na utoaji wa matibabu sahihi kwa watoto wenye tatizo 
hilo.
Kadhalika,
 Waziri Ummy alisema bado kuna hospitali chache zenye uwezo wa kutoa 
huduma ya matibabu ya utapiamlo mkali. Juhudi zinaendelea kuhakikisha 
hospitali zote nchini zinajengewa uwezo wa kutoa huduma hizo muhimu ili 
kuokoa maisha ya watoto walioathirika na utapiamlo mkali.
IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU






No comments:
Post a Comment