WAZIRI
 wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kangi Lugola amewataka wananchi wa Kakonko 
wanaolima jirani na Kambi ya Wakimbizi ya Mtendeli, pamoja na kambi 
zingine zote zilizopo mkoani Kigoma waendelee kulima bila kuomba kibali 
chochote kama ilivyoagizwa awali.
Waziri
 Lugola amefuta utaratibu huo wa utoaji wa vibali kwa ajili ya 
kuruhusiwa kwenda kulima katika maeneo hayo, baada ya wananchi wilayani 
humo kuulalamikia utaratibu huo ambao walisema unawafanya wasiwe huru na
 unawachelewesha kuendeleza shughuli zao za kilimo kama ilivyokua awali.
Akizungumza
 katika mkutano wa hadhara uliohudhuriwa na mamia ya wananchi mjini 
Kakonko, Mkoani Kigoma, jana, Lugola alisema Serikali ya Awamu ya Tano 
haitaki wananchi wake wanyanyaswe, wananchi wanapaswa kua huru katika 
nchi yao.
 “Naagizia
 huu utaratibu ufutwe na wananchi wawe huru kwenda kulima katika maeneo 
ambayo yapo jirani na hiyo kambi pamoja na kambi zinginezo, na pia 
wasisumbuliwe na mtu yeyote, ” alisema Lugola.
Pia
 Waziri Lugola alielekeza baadhi ya wananchi ambao hawajalipwa fidia 
wakati mashamba yao yalipochukuliwa kwa ajili ya kuanzisha kambi hiyo 
wafanyiwe uhakiki ili waweze kulipwa haki zao.
Hata
 hivyo, Mratibu wa Idara ya Wakimbizi Kanda ya Kigoma, Tony Laiser 
ambaye alikuwepo katika mkutano huo alipokea maagizo hiyo na kuahidi 
kuyatekeleza.
Aidha,
 kabla ya mkutano huo wa hadhara, Waziri Lugola alizungumza na  
watendaji waliopo katika wizara yake mkoani humo na alisema Serikali 
imepeleka mafunzoni vijana 1,500 kwaajili ya kujiunga na Jeshi la polisi
 pamoja na kuagiza magari kwa ajili doria.
Pia
 aliwataka watendaji hao kufanya kazi kwa bidii kwani serikali yao ipo 
na inawajali na pia itahakikisha inatatua kero zao ambazo zinawakabili 
ikiwemo ukosefu wa majengo, upungufu wa vitendea kazi na uhaba wa askari
 katika sehemu mbalimbali nchini.






No comments:
Post a Comment