Waziri Lugola Afuta Utaratibu Wa Utoaji Vibali Kwa Wananchi Wanaolima Jirani Na Kambi Za Wakimbizi Nchini

WAZIRI wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kangi Lugola amewataka wananchi wa Kakonko wanaolima jirani na Kambi ya Wakimbizi ya Mtendeli, pamoja na kambi zingine zote zilizopo mkoani Kigoma waendelee kulima bila kuomba kibali chochote kama ilivyoagizwa awali.

Waziri Lugola amefuta utaratibu huo wa utoaji wa vibali kwa ajili ya kuruhusiwa kwenda kulima katika maeneo hayo, baada ya wananchi wilayani humo kuulalamikia utaratibu huo ambao walisema unawafanya wasiwe huru na unawachelewesha kuendeleza shughuli zao za kilimo kama ilivyokua awali.

Akizungumza katika mkutano wa hadhara uliohudhuriwa na mamia ya wananchi mjini Kakonko, Mkoani Kigoma, jana, Lugola alisema Serikali ya Awamu ya Tano haitaki wananchi wake wanyanyaswe, wananchi wanapaswa kua huru katika nchi yao.

 “Naagizia huu utaratibu ufutwe na wananchi wawe huru kwenda kulima katika maeneo ambayo yapo jirani na hiyo kambi pamoja na kambi zinginezo, na pia wasisumbuliwe na mtu yeyote, ” alisema Lugola.

Pia Waziri Lugola alielekeza baadhi ya wananchi ambao hawajalipwa fidia wakati mashamba yao yalipochukuliwa kwa ajili ya kuanzisha kambi hiyo wafanyiwe uhakiki ili waweze kulipwa haki zao.

Hata hivyo, Mratibu wa Idara ya Wakimbizi Kanda ya Kigoma, Tony Laiser ambaye alikuwepo katika mkutano huo alipokea maagizo hiyo na kuahidi kuyatekeleza.

Aidha, kabla ya mkutano huo wa hadhara, Waziri Lugola alizungumza na  watendaji waliopo katika wizara yake mkoani humo na alisema Serikali imepeleka mafunzoni vijana 1,500 kwaajili ya kujiunga na Jeshi la polisi pamoja na kuagiza magari kwa ajili doria.

Pia aliwataka watendaji hao kufanya kazi kwa bidii kwani serikali yao ipo na inawajali na pia itahakikisha inatatua kero zao ambazo zinawakabili ikiwemo ukosefu wa majengo, upungufu wa vitendea kazi na uhaba wa askari katika sehemu mbalimbali nchini.
Share:

No comments:

Post a Comment

IDADI YA WASOMAJI

TUSIKILIZE LIVE KUPITIA TUNEIN

UNGANA NASI FACEBOOK HAPA

10 ZILIZOSOMWA ZAIDI

Labels

Blog Archive