Rais
 John Magufuli ameagiza wafiwa wote waliopoteza ndugu zao kwenye ajali 
ya kivuko cha Mv Nyerere kupata Sh 1 milioni baada ya awali kupewa Sh 
500,000 kila mmoja.
Hata hivyo watu 41 walionusurika kwenye ajali hiyo nao watapewa Sh1 milioni kila mmoja.
Fedha hizo zinatokana na michango ya kampuni, watu na taasisi mbalimbali wanaoendelea kujitokeza kuchangia waathirika hao.
Awali,
 familia za waliopoteza maisha kwenye ajali hiyo iliyotokea Alhamisi 
iliyopita walipewa Sh500,000 kwa kila mtu aliyefariki, fedha ambazo 
zimepatikana kutokana na michango ya Watanzania, kampuni na taasisi 
mbalimbali.
Akizungumza
 na vyombo vya habari jana kisiwani Ukara wilayani Ukerewe, Waziri wa 
Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Isaac Kamwelwe alisema leo wataanza 
kutoa fedha hizo kama walivyoagizwa na Rais Magufuli kwa familia za 
marehemu na wote walionusurika.
“Rais
 ameniagiza niwaambie kwamba fedha kwa waliopoteza ndugu zao na wale 41 
walionusurika, sasa watapata Sh1 milioni kila mmoja. Kuanzia kesho (leo)
 tutaanza kutoa fedha hizo, wapeni taarifa,” alisema Kamwelwe.
Alisema
 kiwango cha fedha kilichokusanywa mpaka jana jioni ni Sh397 milioni 
ambazo zimetolewa na watu na taasisi mbalimbali. Alisema Rais Magufuli 
amesema fedha hizo ni za wananchi walioathirika na ajali hiyo.
Waziri
 huyo alisema mpaka kufikia jana jioni, miili miwili ya watoto 
ilipatikana wakati kazi ya kukiinua kivuko hicho ikiendelea na kufanya 
idadi ya waliopoteza maisha kwenye ajali hiyo kufikia 226.
Kuhusu
 kurudisha hali ya usafiri katika kisiwa hicho, Kamwelwe alisema leo au 
kesho kitapelekwa kivuko kingine kinachoitwa Mv Temesa ambacho kiko 
Mwanza kwa ajili ya kutoa huduma wakati shughuli ya kukiinua kivuko cha 
Mv Nyerere ikiendelea.






No comments:
Post a Comment