Wizara
 ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki imeendelea kupokea 
salamu za rambirambi kutoka kwa marais, mawaziri wakuu wa mataifa 
mbalimbali duniani kwenda kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, 
Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, kufuatia ajali ya kuzama kwa
 kivuko cha MV Nyerere iliyotokea kwenye Ziwa Victoria, Mkoani Mwanza 
tarehe 20 Septemba, 2018 na  kusababisha vifo, majeruhi na upotevu wa 
mali.
Baadhi
 ya salamu zilizopokelewa ni pamoja na kutoka kwa Rais wa Kenya, 
Mheshimiwa Uhuru Kenyatta, Rais wa Urusi, Mheshimiwa Vladmir Putin, Rais
 wa China, Mheshimiwa Xi Jinping, Rais wa Ujerumani, Mheshimiwa 
Frank-Walter Steinmeier, Rais wa Saharawi, Mheshimiwa Brahim Ghali, 
Mtawala wa Kuwait, Mtukufu Sheikh Sabah Al-Ahmad al Jaber Al-Sabah, Baba
 Mtakatifu, Papa Francis, Rais wa Italia, Mheshimiwa Sergio Mattarella, 
Rais wa Uturuki, Mheshimiwa Recep Tayyip Erdogan, Rais wa Finland, 
Mheshimiwa Sauli Niinistö, Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, 
Mheshimiwa Joseph Kabila Kabange na Rais wa Jamhuri ya Sudan, Mheshimiwa
 Omar Hassan Ahmed Al-Bashir.  
Viongozi wengine ni Waziri Mkuu wa Israel, Mheshimiwa Benjamin Netanyahu, na Waziri Mkuu wa Sweden, Mheshimiwa Stefan Löfven.
Viongozi
 hao wameeleza kusikitishwa kwao na taarifa za vifo vilivyosababishwa 
na  ajali hiyo na kuwatakia majeruhi kupona haraka.
Sehemu
 ya nukuu za salamu hizo zinasema “Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe 
Magufuli, nilipokea kwa huzuni na masikitiko makubwa taarifa za ajali ya
 kivuko cha MV Nyerere iliyosababisha vifo vya watu wengi, majeruhi na 
wengine kutojulikana walipo. Kwa niaba ya Serikali na wananchi wa Kenya 
naomba upokee na kufikisha salamu zetu za rambirambi kwa wafiwa na 
wananchi wote wa Tanzania kufuatia ajali hiyo na tunawaombea majeruhi 
wote wapone haraka” ni sehemu ya nukuu ya salamu kutoka kwa Mheshimiwa 
Rais Kenyatta
“Mheshimiwa
 Rais Dkt. John Pombe Magufuli, nilishtushwa na taarifa za ajali hiyo 
mbaya iliyotokea Mkoani Mwanza. Kwa niaba ya Serikali ya China, wananchi
 na mimi binafsi natoa pole kwa wafiwa wote na majeruhi” inasema sehemu 
ya salamu kutoka kwa Rais wa China, Mheshimiwa Xi Jinping.
Naye
 Rais wa Urusi, Mheshimiwa Putin amesema “Mheshimiwa Rais Dkt. John 
Pombe Magufuli, tafadhali naomba upokee salamu zangu za rambirambi 
kufuatia ajali iliyotokea. Naomba salamu hizi ziwafikie wafiwa wote na 
ninawaombea majeruhi wapone haraka”
Aidha,
 Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki imepokea 
salamu za rambirambi kutoka kwa balozi mbalimbali zinazowakilisha nchi 
zao hapa nchini pamoja na mashirika ya kimataifa yaliyopo nchini, 
ikiwemo ubalozi wa Marekani, ubalozi wa Ufaransa, ubalozi wa Sudan 
Kusini, Ubalozi wa Falme za Kiarabu (UAE), Serikali ya Brazil, Ubalozi 
wa Cuba, ubalozi wa Nigeria na salamu kutoka kwa Mratibu Mkazi wa 
Mashirika ya Kimataifa nchini.
Wakati
 huohuo, Wizara imepokea salamu za rambirambi kutoka kwa mabalozi 
wanaowakilisha Tanzania kwenye nchi mbalimbali. Salamu zilizopokelewa 
zinatoka kwa mabalozi wote wa Tanzania  katika nchi za Qatar, Ufaransa, 
Uingereza, Uholanzi, Afrika Kusini, Sweden, Nigeria, Burundi, Uganda, 
Kenya, Ubelgiji, Zambia, Msumbiji, China, Japan, Brazil, Comoro, 
Algeria, Sudan,  Canada,
Kadhalika
 tumepokea salamu kutoka kwenye balozi zetu zilizoko Marekani, Uturuki, 
Rwanda, Umoja wa Falme za Kiarabu, Misri, Kuwait, Saudi Arabia, Jamhuri 
ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), Zimbabwe, Malawi, Uswisi, India, Italia,
 Jamhuri ya Korea, Urusi, Israel, Ethiopia, Ujerumani, Oman na Malaysia.
Baadhi
 ya nukuu ya salamu za rambirambi za mabalozi hao zinasomeka kama 
ifuatavyo “Inna Lillah Wainna Illah Rajiuon.  Kwa  niaba  ya  Ubalozi  
Abuja  na  Watanzania  waliopo  katika  eneo  letu  la  uwakilishi,  
tunatoa  pole  kwa  Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa 
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,  familia  na  Watanzania  kwa  ujumla  
kwa  msiba  mkubwa  uliotufika.  Mwenyezi  Mungu  atupe  subira  na  
faraja  katika  kipindi  hiki  cha  majonzi  na  aziweke  roho  za  
marehemu  mahali  pema  na  majeruhi  wapone  haraka, Amin  Amin,”  ni 
kauli yake Mheshimiwa Muhidin Ally Mboweto, Balozi wa Tanzania nchini 
Nigeria.
Naye
 Balozi wa Tanzania nchini Sweden, Mheshimiwa Dkt. Wilbroad Slaa anasema
 “kwa niaba ya wenzangu katika kituo cha Stockholm tunatoa pole za dhati
 kwa Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya 
Muungano wa Tanzania, ndugu na familia zote zilizoguswa na msiba huu 
mkubwa. Mwenyezi Mungu azilaze roho za marehemu mahali pema peponi na 
kuwatia nguvu na ujasiri ndugu wote walioguswa na msiba huu”.
Kwa
 upande wake Mwakilishi wa Kudumu wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa 
Mheshimiwa Balozi Modest Mero alisema haya; “Ubalozi wa New York tunatoa
 pole kwa ajali mbaya ya Meli ya MV Nyerere iliyopelekea wengi kupoteza 
maisha na wengi kuumia.  Tunawaombea marehemu pumziko la milele na wote 
waliojeruhiwa wapone haraka.”
Balozi
 wa Tanzania nchini China, Mheshimiwa Mbelwa Kairuki alieleza masikitiko
 yake kwa kusema kuwa “nasi huku Beijing tunaungana na wenzetu kutoa 
pole kwa Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Watanzania na 
wanafamilia walioguswa msiba huu mzito. Mwenyezi Mungu awape nguvu na 
awajalie moyo wa subira wakati wote mnaposhughulika na msiba huo.
“Japan
 na diaspora yetu tunatoa pole kwa Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph 
Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Watanzania wote kwa
 msiba huu uliotokana na kuzama kwa kivuko. Mungu atupe nguvu wote 
tuliobaki na awape pumziko la amani wenzetu waliotutangulia. Kwa 
majeruhi tunawaombea wapone haraka na wavumilie mstuko huu mkubwa katika
 maisha yao. Marehemu wapumzike kwa amani”. Hizi ni salamu kutoka kwa 
Mheshimiwa Mathias Chikawe, balozi wa Tanzania nchini Japan.
Kwa
 upande wake, Balozi wa Tanzania nchini Abu Dhabi alisema haya; “Ubalozi
 wa Tanzania Abu Dhabi, tumepokea kwa masikitiko makubwa taarifa za 
ajali ya MV Nyerere.Kwa niaba ya watumishi wote wa Ubalozi, tunatoa 
mkono wa pole kwa Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Joseph Magufuli na 
Watanzania wenzetu wote kwa msiba huu mkubwa. Mwenyezi Mungu awajaalie 
marehemu wapumzike mahali pema na awajaalie majeruhi kupona mapema. 
Amin”.
Naye
 Balozi wa Tanzania nchini Uingereza, Mheshimiwa Dkt. Asha-Rose Migiro 
akieleza kuguswa na ajali hiyo alitoa kauli hii “Ubalozi wa Tanzania 
London unajumuika na Watanzania wenzetu kutoa pole kwa Mheshimiwa Rais 
Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, familia na ndugu wa wale wote 
waliopatwa na msiba kutokana na ajali hii. Tunawaombea majeruhi wapone 
haraka na warejee katika shughuli zao za kujikimu na kulijenga taifa 
letu”.
Kwa
 upande mwingine, Wizara imepokea salamu za rambirambi kutoka Baraza la 
Diaspora wa Tanzania ulimwenguni kote (TDC Global) ambao wameeleza 
masikitiko makubwa kufuatia ajali hiyo mbaya. Sehemu ya ujumbe wao 
unasomeka kama ifuatavyo; “TDC Global, kwa masikitiko makubwa, inatoa 
salamu za rambirambi kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, 
Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli na Watanzania wote, ndugu, 
jamaa na marafiki kwa vifo vilivyotokana na ajali ya kuzama kwa kivuko 
cha MV. Nyerere kinachofanya safari zake kati ya visiwa vya Bugorora na 
Ukara katika Ziwa Victoria. Kama TDC Global, tunaungana na Watanzania 
wote katika kuomboleza msiba huu mzito kwa taifa letu. Pia tunatoa pole 
kwa majeruhi wote na kuwaombea wapone haraka”.






No comments:
Post a Comment