Serikali yapiga MARUFUKU matangazo ya uzazi wa mpango


Serikali  imesitisha matangazo yanayohamasisha uzazi wa mpango yanayorushwa kwenye runinga na redio mbalimbali nchini mpaka itakapotangazwa tena.

Sitisho hilo limetolewa katika taarifa iliyotolewa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dk. Mpoki Ulisubisya kwenda kwa Shirika la Msaada la Marekani (USAID).

Shirika hilo ndilo linalofadhili mradi wa Tulonge Afya unaotoa matangazo hayo ya kuhamasisha uzazi wa mpango kwenye vyombo vya habari.

Barua hiyo iliyosambaa mitandaoni, inaeleza kuwa serikali inatambua mchango na juhudi za shirika hilo katika kuboresha uzazi wa mpango.

Inaeleza kuwa wizara inakusudia kufanya marejeo ya maudhui yote ya matangazo kwenye runinga na redio kwa ajili ya uzazi wa mpango.

“Hivyo unaombwa kusimamisha mara moja kutangaza na kuchapisha maudhui yoyote yale ya uzazi wa mpango kwenye vyombo vya habari mpaka itakavyoamuliwa vinginevyo,” inaeleza taarifa hiyo.

Akiwahutubia mamia ya watu Septemba 9, mjini Meatu Mkoani Simiyu, wiki mbili zilizopita, Rais John Magufuli alisema Watanzania waendelee kuzaa, lakini wachape kazi ili kukidhi mahitaji ya watoto wanaowazaa.

Alisema anafahamu Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu angependa kuongelea mambo ya uzazi wa mpango, lakini mengine yeye (Magufuli) hakubaliani nayo.

“Najua Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu, angependa kuongelea mambo ya uzazi wa mpango hapa, lakini mimi mengine huwa sikubaliani nayo sana, utapangiwaje kuzaa...kwa hiyo katika kushauriwa mengine tukubali na mengine tukatae tutumie msemo wa mzee Jakaya Kikwete ‘Ukiambiwa changanya na za kwako’ kuzaa ni muhimu,” alisema.

Katika mkutano huo Rais Magufuli aliwaeleza wananchi kuwa katika mataifa ya kigeni aliyowahi kuishi hakuwahi kusikia wimbo wa uzazi wa mpango.

“Mimi Ulaya nimekaa, nafahamu madhara ya kutokuzaa, nchi gani sijakwenda, Japan nimekaa, Uingereza nimekaa mwaka mzima, Ujerumani nimekaa, Canada nimekaa na nikachaguliwa kuwa Mwenyekiti Mwenza wa Mawaziri Ardhi Duniani, nimekaa Denmark, Norway, China nimefika sasa utanidanganya wapi,” alisema.
Share:

No comments:

Post a Comment

IDADI YA WASOMAJI

TUSIKILIZE LIVE KUPITIA TUNEIN

UNGANA NASI FACEBOOK HAPA

10 ZILIZOSOMWA ZAIDI

Labels

Blog Archive