Waziri wa Nishati autaka Mgodi wa GGM kutumia umeme wa gridi ili walipe kodi stahiki.

WAZIRI Nishati Dk. Medard Kalemani amesema kukamilika kwa mradi wa ujenzi wa mtambo wa kupoza umeme unaotarajiwa kujengwa Geita, kutawezesha serikali kupeleka umeme wa gridi ya taifa katika Mgodi wa Dhahabu wa Geita (Geita Gold Mine – GGM) na kuondoa sababu ya wao kutokulipa kodi stahiki kwa serikali kwa kigezo cha kutumia mafuta katika uzalishaji.
 
Akikagua eneo utakapojengwa mtambo huo, nje kidogo ya mji wa Geita, Desemba 31 mwaka huu, Waziri Kalemani alisema mtambo huo utafua umeme wa megawati 100 hivyo pamoja na kuwanufaisha wananchi wa Geita na maeneo jirani; utatosheleza pia mahitaji ya mgodi husika ambayo ni takribani megawati 25.
 
“Ni matumaini yangu, kufikia Desemba 2019, GGM watakuwa wameanza kutumia umeme wa gridi ya taifa ili waanze kulipa kodi stahiki kwa serikali. Waache kupata msamaha wa kodi wanaopata sasa kutokana na kuingiza mafuta wanayotumia kuendeshea shughuli zao mgodini,” alisema Waziri.
 
Waziri Kalemani aliongeza kwamba, kuwaunganisha GGM na umeme wa gridi, kutakamilisha azma ya serikali kuwaunganishia umeme wachimbaji wa madini wakubwa wote nchini kwani kwa sasa ni mgodi huo pekee uliobaki.
 
Alimtaka Meneja wa TANESCO Mkoa wa Geita, Mhandisi Joackim Ruweta kuwapa taarifa uongozi wa mgodi huo ili waanze kufanya maandalizi ya kuupokea umeme kwenye miundombinu yao.
 
Akizungumzia kuhusu mradi wenyewe, Waziri Kalemani alieleza kuwa serikali imetoa takribani shilingi bilioni 23 kwa ajili ya kuujenga ili kuboresha hali ya upatikanaji umeme kwa wananchi wa Geita na maeneo jirani.
 
Alisema mradi unahusisha kusafirisha umeme mkubwa kutoka Bulyanhulu, umbali wa kilomita 55 hadi Geita.
 
Aidha, alisema kuwa taratibu zote za maandalizi zimekamilika hivyo akamtaka mkandarasi atakayetekeleza mradi huo, ambayo ni kampuni ya CAMC Engineering kutoka China kuanza mara moja shughuli za ujenzi, ambao kwa mujibu wa mkataba utakamilika ndani ya kipindi cha miezi 17.
 
“Pamoja na kuwa mkataba unabainisha muda wa kukamilisha ujenzi ni miezi 17 lakini tumekubaliana na mkandarasi ajitahidi kukamilisha ndani ya miezi 12,” alifafanua Waziri.
 
Akizungumzia majukumu ya mkandarasi kwa mujibu wa mkataba, Waziri Kalemani alisema yanajumuisha ujenzi wa mtambo wenyewe wa kupoza umeme katika eneo la Mpomvu, nje kidogo ya mji wa Geita, ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme kutoka Bulyanhulu hadi eneo la mtambo, umbali wa kilomita 55 pamoja na kazi ya kusambaza umeme kwenye vijiji 11 vinavyopitiwa na mradi vikiwemo vya Nyantororo na Buyagu.
 
Waziri aliagiza mambo kadhaa yafanyike katika utekelezaji wa ujenzi wa mradi huo ambayo ni pamoja na kujenga uzio kuzungushia eneo husika kwa sababu za kiusalama pamoja na kuepusha watu kuvamia eneo husika na kujenga makazi.
 
Pia, aliagiza kuanza mara moja kwa kazi za kusafisha eneo husika pamoja na kutoa elimu kwa wananchi ambako mradi unapita ili wajue namna ya kujiandaa kuupokea mradi husika.
 
Waziri Kalemani alikuwa katika ziara ya kazi kukagua utekelezaji wa miradi ya umeme ambapo mbali na kukagua eneo utakapojengwa mtambo huo, aliwasha umeme Katoro na Buseresere katika vijiji kadhaa pamoja na kuzungumza na wananchi.
Share:

No comments:

Post a Comment

IDADI YA WASOMAJI

TUSIKILIZE LIVE KUPITIA TUNEIN

UNGANA NASI FACEBOOK HAPA

10 ZILIZOSOMWA ZAIDI

Labels