Tamko La Wizara Ya Afya Kulaani Vitendo Vya Ukatili Wa Watoto Majumbani Ikiwemo Mtoto Kufungiwa Kabatini

Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto inalaani na kukemea vikali vitendo vya ukatili dhidi ya watoto vinavyoendelea kujitokeza nchini. Vitendo hivi vinafanywa na kuhusisha ndugu na walezi wa karibu wa wataoto hivyo kuzua hofu kubwa kwa watoto na jamii kwani vinaathiri malezi na makuzi ya awali ya watoto kwa kutozingatia haki zao za msingi.

Mapema wiki hii, imeripotiwa  mwalimu wa shule ya msingi jijini Dodoma  (jina limehifadhiwa) ambaye anatuhumiwa kumfungia mtoto mdogo ndani ya kabati kwa kipindi kirefu na kusababisha afya ya mtoto huyo kudhohofika. Mwalimu huyo anatuhumiwa pia kumfanyia vitendo vya ukatili mama mzazi wa mtoto  huyo kwa kumpiga na kumsababishia maumivu mwilini yaliyopelekea binti huyo na mtoto wake kulazwa.

Kipekee, Wizara inawapongeza wanajamii wote walioibua tukio hili na kuwezesha Jeshi la Polisi kumkamata mtuhumiwa kwa ajili ya uchunguzi ili Sheria iweze kuchukua mkondo wake. TunaaminiJeshi la Polisi watafanya upelelezi wa tukio hili kwa weledi mkubwa ili hatua stahiki za kisheria ziweze kuchukuliwa.

Matukio ya ukatili wa watoto yanapotokea majumbani yanarudisha nyuma jitihada za Serikali za kulinda na kuendeleza haki na ustawi wa watoto katika ngazi ya familia ambayo ndio kitovu cha jamii wakiwemo na watoto.

Kufuatia kitendo hicho kilichofanywa na mwalimu wa shule ya msingi ambaye ni mlezi wa watoto, Wizara inawataka wazazi, walezi na jamii kuzingatia wajibu wa ulinzi wa watoto ili kuwahakikishia usalama wao katika maeneo ya majumbani, shuleni, mtaani, njiani na katika jamii kwa ajili ya kutekeleza lengo la kupunguza matukio ya ukatili kwa asilimia 50 ifikapo mwaka 2021/2022.

Aidha, Wizara inatoa rai kwa jamii na wananchi wema kuwa makini na matumizi ya mitandao ya kijamii ili kuepuka makosa ya kisheria yanayoweza kutokea kwa kusambaza, kuchapisha na kupiga picha za watoto ambao ni wahanga wa ukatili na kuziweka wazi kinyume na Sheria ya Mtoto Na. 21 ya Mwaka 2009.

Wizara inatoa pole kwa wazazi, ndugu, marafiki na familia ya mtoto aliyefanyiwa ukatili huo. Tunawaomba wanajamii kuendelea kutoa ushirikiano katika kufichua vitendo vyote vya ukatili dhidi ya watoto vinavyojitokeza katika maeneo yao. Aidha, katika kipindi hiki ambapo uchunguzi unaendelea kufanyika tunaomba pawe na utulivu na uvumilivu ili kutoa nafasi kwa vyombo vya dola kufanya uchunguzi kwa makini na Sheria iweze kuchukua mkondo wake.

Imetolewa na
Kitengo cha Mawasiliano Serikalini
Wizara ya Afya Maendeleo ya Jamii Jinsia Wazee na Watoto
(Idara Kuu Maendeleo ya Jamii)
02/01/2019
Share:

No comments:

Post a Comment

IDADI YA WASOMAJI

TUSIKILIZE LIVE KUPITIA TUNEIN

UNGANA NASI FACEBOOK HAPA

10 ZILIZOSOMWA ZAIDI

Labels