Wamiliki Wa Nyumba za Kupanga Wapewa ONYO

Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Angeline Mabula, amewaonya baadhi ya watu wanaomiliki nyumba na kuendelea kuwatoza wapangaji wao kodi za miezi sita na mwaka mmoja, kinyume na maelekezo ya serikali, kuheshimu maelekezo hayo.

Naibu waziri huyo alitoa onyo hilo jana, alipokuwa akihojiwa na kituo kimoja cha redio na kuwataka wenye nyumba hao kuwasaidia mwananchi wa kawaida.

"Lengo na madhumuni ni kumsaidia Mtanzania wa kawaida ambaye hutegemea kipato cha mshahara ama biashara, ili aweze kufanya bajeti yake kama kulipa nyumba ama matumizi mengine. Unapomwambia alipe miezi sita ama mwaka mmoja unamtaka atafute kipato cha ziada akuridhishe mwenye nyumba halafu mpangaji abaki na madeni kitu ambacho hakimsaidii Mtanzania," alisema.

Alisema mkakati wa serikali ni kuweka vitu katika usawa ili kuwawezesha wapangaji.

Mabula alisema sheria kuhusu suala hilo bado haijatungwa, lakini ni vizuri wenye nyumba wakajiandaa mapema ili sheria itakapopitishwa wawe wameshazoea.

"Kwa sasa ipo katika mchakato haujapelekwa muswada wa kusomwa bungeni kwa kuwa bado hatujachukua maoni ya wadau, lakini ndani ya mwaka wa fedha unaokuja itakuwa tayari maana imeonekana ni hitaji kubwa," alisema.

Mwishoni mwa mwaka juzi, Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi, aliagiza watu wanaomiliki nyumba za kuzipangisha, kuacha kuwatoza wapangaji wao kodi za miezi sita hadi mwaka mmoja ili wasio na uwezo waweze kumudu maisha.

Waziri Lukuvi, wakati akitoa agizo hilo, alisema mpangaji anatakiwa kulipa kodi kila mwezi labda atake mwenyewe kulipa kwa miezi zaidi ya mmoja.
Share:

No comments:

Post a Comment

IDADI YA WASOMAJI

TUSIKILIZE LIVE KUPITIA TUNEIN

UNGANA NASI FACEBOOK HAPA

10 ZILIZOSOMWA ZAIDI

Labels