Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu imewahukumu kifungo cha miaka 28 jela kila mmoja wafanyakazi wawili wa Benki ya NMB.
Wafanyakazi
 hao, Mtoro Midole na Daudi  Kindamba wamehukumiwa jana Jumatatu Oktoba 
Mosi, 2018 baada ya kupatikana na hatia katika mashtaka ya wizi, 
utakatishaji wa fedha na kuisababishia benki hiyo hasara ya Sh1.03 
bilioni.
Hukumu hiyo iliandaliwa na hakimu mkazi mwandamizi, Godfrey Mwambapa na kusomwa na hakimu Mkuu, Wanjah Hamza.
Akisoma
 hukumu hiyo, Wanjah chini ya sheria ya kanuni ya adhabu aliamuru 
washtakiwa hao mbali na adhabu ya vifungo hivyo pia walipe kiasi cha 
hicho cha fedha.
John
 Kikoka aliyekuwa miongoni mwa washtakiwa hao, aliachiwa huru  baada ya 
mashahidi 21 wa  upande wa mashtaka katika kesi hiyo ya jinai namba 118 
ya 2014, kushindwa kuthibitisha mashtaka dhidi yake.
Hakimu
 Wanjah akiisoma hukumu hiyo, alisema washtakiwa Midole na Kindamba 
wamekutwa na hatia katika shtaka la wizi ambapo aliwahukumu kifungo cha 
miaka mitano jela kila mmoja.
Katika
 shtaka la kutengeneza miamala ya uongo, ambalo linamkabili mshtakiwa 
Midole pekee, Hakimu Wanjah alisema atatumikia kifungo cha miaka 10 
jela.
Katika
 mashtaka ya utakatishaji wa fedha, Hakimu Wanjah alisema mshtakiwa 
Midole na Kindamba wamekutwa na hatia katika shtaka moja moja, kati ya 
mawili mawili yanayowakabili hivyo kila mshtakiwa atalipa faini katika 
kosa moja Sh500 milioni hivyo katika mashtaka mawili kila mshtakiwa 
anapaswa kulipa Sh1 bilioni ama kutumikia kifungo cha miaka mitano jela.
Hakimu
 Wanjah katika shtaka la kusababisha hasara ya Sh1.03 bilioni kwa benki 
ya NMB, aliamuru kila mshtakiwa kulipa faini ya Sh5 milioni ama 
kutumikia kifungo cha miaka mitano jela.
Awali,
 kabla ya Hakimu Wanjah kusoma hukumu hiyo, wakili wa Serikali 
mwandamizi Kishenyi Mutalemwa aliieleza  mahakama hiyo kuwa hana 
kumbukumbu za makosa ya nyuma ya washtakiwa hao.
Wakili 
 Kishenyi aliiomba mahakama hiyo kutoa adhabu ya kiwango cha juu kwa 
washtakiwa hao, katika kila kosa walilotiwa hatiani kama Matakwa ya 
sheria yanavyotaka. 
Alibainisha
 lengo la  kuomba adhabu hiyo ni mshtakiwa wa kwanza ambaye ni 
mfanyakazi wa benki ya NMB na  amekasimiwa na kuaminika kutunza fedha za
 wananchi na kwamba kosa la wizi na utakatishaji wa fedha imekuwa ni 
tishio kwa uchumi nchini hasa ukizingatia kiwango kikubwa cha fedha 
kilichohusika katika kesi hiyo. 
Pia, aliiomba mahakama itoe amri kwa washtakiwa hao kurudisha fedha walizoisababishia hasara benki ya NMB.
Hakimu
 Wanjah alipowataka washtakiwa hao waongee chochote kabla ya kupewa 
adhabu hizo, Midole aliiomba Mahakama iwafikirie kwani wamekaa mahabusu 
kwa miaka minne kwa sababu mashtaka yaliyokuwa yakiwakabili ni miongoni 
mwa  mashtaka yasiyo na dhamana kwa mujibu wa sheria.
Pia, aliiomba mahakama impatie nakala ya mwenendo wa shauri hilo na nakala ya hukumu kwa sababu anakusudia kukata rufaa.
Kindamba
 aliomba mahakama iangalie muda waliokaa mahabusu huku akiomba kupatiwa 
mwenendo wa shauri hilo na nakala ya hukumu kwa kuwa anakusudia kukata 
rufaa.






No comments:
Post a Comment