WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa ametoa siku mbili kwa Kaimu Afisa Elimu (Msingi) wa wilaya ya Muleba, mkoani Kagera Bw. Bukuru Malembo awe amepeleka walimu wawili katika shule ya msingi iliyoko kwenye kitongoji cha Rwenzige kwa kuwa haina mwalimu hata mmoja.
Shule
 hiyo yenye madarasa wawili na ofisi moja ya mwalimu ina jumla wanafunzi
 216 wa darasa la awali hadi la nne, ilijengwa na wananchi ambapo 
wanafunzi wake wanafundishwa na mwananchi mmoja aliyemua kujitolea ili 
kuwapunguzia watoto kutembea umbali wa kilomita 16 kwenda kusoma katika 
shule ya kijiji cha Kiteme.
Waziri
 Mkuu alitoa agizo hilo jana (Jumatatu, Oktoba 8, 2018) baada ya 
wanafunzi wa shule hiyo kuwasilisha malalamiko yao kwa njia ya bango 
wakati akizungumza na wananchi katika mkutano wa hadhara uliofanyika 
kwenye kiwanja cha kituo cha afya Kimeya, baada ya kukagua majengo ya 
kituo hicho.
“Haiwezekani
 watoto wadogo wenye umri wa kuanzia miaka mitano wakatembea umbali wa 
kilomita 16 kwenda shule wakati katika kitongoji chao kuna shule yenye 
madarasa mawili na chumba kimoja cha ofisi ya mwalimu na Afisa Elimu 
hadi sasa hajapeleka walimu na kumuachia mwalimu Benson (kijana ambaye 
si mwalimu ila anajitolea kufundisha) akifundisha wanafunzi hao peke 
yake.”
Waziri
 Mkuu alimuagiza Afisa Elimu huyo ahakikishe ifikapo Jumatano (Oktoba 
10, 2018) saa nne asubuhi awe ameshawapeleka walimu hao katika shule 
hiyo ya msingi ili waweze kuwafundisha wanafunzi hao na kisha Mkuu wa 
wilaya hiyo, Mhandisi Richard Ruyango awasilishe taarifa ya utekelezaji 
wa agizo hilo ofisini kwake. “Walimu wengi mmewaacha katika shule za 
barabarani huku za vijijini zikiwa hazina walimu.”
Kwa
 upande wake, Bw. Benson Bukerebe (29) maarufu mwalimu Benson alisema 
yeye kitaaluma si mwalimu bali ni mhitimu wa kidato cha nne, alimua 
kuanzisha darasa kwa ajili ya kuwafundisha wanafunzi hao kwani alikuwa 
akiwahurumia kwa sababu baadhi yao hawakuwa na uwezo wa kutembea umbali 
wa kilomita 16 hadi iliko shule ya msingi ya Kiteme.
Kijana
 huyo alisema kwa muda wote huo ameweza kumudu kuwafundisha wanafunzi 
hao kwa kutumia vitabu vya kuazima kutoka shule mbalimbali za msingi, 
lengo ni kuhakikisha watoto wenye umri wa kuanza shule katika kitongoji 
chao wanapata fursa ya elimu ambayo ni haki yao ya msingi.
Katika
 hatua nyingine,Waziri Mkuualisema Serikali imeweka sheria kali ili 
kuwalinda watoto wa kike na wanatakiwa kuheshimiwa katika jamii kwa 
kuachwa waendelee na masomo yao bila ya usumbufu wa aina yoyote na 
atakayebainika kukatisha masomo yao atachukulia hatua kali za kisheria.
Alisema
 Serikali  itatoa adhabu kali ya kifungo cha miaka 30 jela kwa mtu 
atakayekatisha elimu ya mtoto wa kike iwe kwa kumuoa, kumpa ujauzo na 
hata ukikutwa naye nyumbani kwako na katika nyumba ya wageni.
“Tukikukuta
 na binti wa shule katika kona isiyoeleweka tunakukamata na kukuchukulia
 hatua za kisheria. Ole wenuvijana, mkibainika mmewapa mimba mabinti 
wanaosoma, adhabu yake ni miaka 30 jela.”
Waziri
 Mkuu alisema kwa wazazi au walezi watakaowaozesha watoto kike ambao 
bado ni wanafunzi na kwa upande wa wazazi watakaomsindikiza mtoto wao wa
 kiume kwenda kuoa mwanafunzi wote watachukuliwa hatua za kisheria.
IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,
JUMANNE, OKTOBA 9, 2018.






No comments:
Post a Comment