Vijana
 saba wenye umri kati ya miaka 21 na 24 leo Jumanne Oktoba 2, 2018 
wamefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu wakikabiliwa na 
shtaka la kuharibu noti za Sh70,000.
Wakili
 wa Serikali, Mwanaamina Kombakono amewasomea mashtaka yao leo, akieleza
 kuwa wanakabiliwa na kesi ya jinai namba 299 ya 2018 mbele ya Hakimu 
Mkazi Mkuu, Hamza Wanjah.
Kombakono
 amewataja washtakiwa hao kuwa ni Vicent Kaduma (24), Rogers Swale (23),
 mwanafunzi Doreen Mwenisongole (22), Kelvin Mgeyekwa (23), Elia 
Chengula (24), Said Sadiq (21) na Ramadhani Selemani (23) wote wakazi wa
 Dar es Salaam maeneo ya Bahari Beach na Kunduchi.
Kombakono
 amedai Septemba 16, 2018 jijini Dar es Salaam, bila ya kuwa na mamlaka 
washtakiwa hao waliharibu kwa kuzikanyaga noti za Sh 70,000 za Benki Kuu
 ya Tanzania (BoT).
Baada ya kusomewa shtaka hilo, washtakiwa wote walikana na upande wa mashtaka ulisema upelelezi wa kesi hiyo bado haujakamilika.
Wakili
 wa upande wa utetezi, Stoki Joackim anayewatetea washtakiwa wote 
aliiomba mahakama iwapatie dhamana wateja wake kwa sababu shtaka 
linalowakabili linadhaminika kwa mujibu wa sheria na kwamba dhamana ni 
haki ya washtakiwa.
Baada
 ya kusikiliza hoja hiyo, Hakimu Wanjah alitoa masharti ya dhamana kwa 
washtakiwa kwa kumtaka kila mmoja  kuwa na wadhamini wawili wenye  barua
 na nakala za kitambulisho na kwamba kila mdhamini asaini bondi ya Sh 2 
milioni.
Washtakiwa wote walifanikiwa kukamilisha masharti hayo ya dhamana na kuachiwa huru.
Kesi hiyo imeahirishwa hadi Novemba 2, 2018 itakapotajwa tena.






No comments:
Post a Comment