TAKUKURU
 Mkoa wa Dodoma jana usiku iliweka mtego na kufanikiwa kumkamata Jacob 
Paul Nyangusi ambaye ni Mhadhiri wa Kitivo cha Sayansi ya Jamii katika 
Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) kwa kosa la kumtaka mwanafunzi wa mwaka wa 
kwanza kingono ili amsaidie katika mitihani ya marudio aliyofanya hivi 
karibuni.
Kosa hili ni kinyume na kifungu cha 25 cha Sheria ya Kuzuia na Kupambana na rushwa Na. 11/2007.
Mhadhiri
 huyo alikamatwa saa tatu usiku katika eneo la nyumba mia tatu kata ya 
Nzuguni jijini Dodoma akiwa chumbani na mwanafunzi huyo. 
Awali
 TAKUKURU ilipokea taarifa za Mhadhiri huyo kutaka rushwa ya ngono kwa 
mwanafunzi wake ambaye jina limehifadhiwa ili amwezeshe kufanya mitihani
 ya marudio baada ya kufeli na pia amsaidie wakati wa usahihishaji.
Baada ya kupokea taarifa hizo TAKUKURU ilifanya uchunguzi wa awali na kuandaa mtego uliofanikisha kukamatwa kwake. 
TAKUKURU
 inaendelea na uchunguzi na mtuhumiwa huyo atafikishwa mahakamani pindi 
kibali cha Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP) kikitolewa.
TAKUKURU
 Mkoa wa Dodoma imekuwa inapokea taarifa za baadhi ya wahadhiri wasio 
waadilifu kuwataka wanachuo hasa wa kike kingono ili wawasaidie katika 
masomo yao.
 Aidha, baadhi wanawafelisha wanafunzi kwa makusudi na baadaye kuwataka rushwa ili warekebishe matokeo yao.
TAKUKURU
 inatoa wito kwa wanafunzi wa kike na wananchi wote kwa ujumla kutoa 
taarifa za vitendo vya rushwa ya ngono wanapokutana navyo.






No comments:
Post a Comment