Mfumo Wa Utambuzi Wa Matukio Ya Binadamu Kuharakisha Maendeleo

SERIKALI inatekeleza Mpango wa Pili wa Maendeleo ya Taifa wa miaka mitano (2016/17- 2020/21) unaolenga katika kuimarisha ustawi na maendeleo ya jamii kwa kuongeza upatikanaji wa huduma bora za jamii ikiwemo elimu, afya na maji.

Ili kufanikisha malengo hayo, Serikali imeweka utaratibu wa kukusanya taarifa muhimu za wananchi wake kupitia takwimu mbalimbali ili kuweza kupanga mipango ya maendeleo.

Taarifa hizo zinazotolewa katika mfumo wa takwimu ikiwemo hali ya vizazi na vifo nchini zinalenga katika kuanisha mahitaji halisi ya wananchi ili kurahisisha uandaaji wa sera na mipango ya maendeleo kulingana na mahitaji na mazingira yaliyopo

Pamoja na jitihada hizo inaelezwa kuwa mfumo  wa usajili, utambuzi na uwekaji wa kumbukumbu wa matukio muhimu ya binadamu  ikiwemo vizazi, vifo, ndoa, talaka na hati za uasili wa watoto umekabiliwa na changamoto mbalimbali kutokana na mifumo ya sheria zilizopo.

Inaelezwa kuwa matukio mengi yanatokea katika ngazi za vjiji, vitongoji, mitaa na kata ambapo watendaji na viongozi wa mamlaka husika wanatambua uwepo wake yameshindwa kuingizwa katika taarifa rasmi kutokana na  Sheria za Serikali za Mitaa kutowapa jukumu la kusajili na kutunza takwimu za matukio hayo.

Wizara ya Katiba na Sheria kupitia Wakala wa Usajili, Ufulisi na Udhamini (RITA) inatekeleza Mkakati wa Taifa wa Usajili wa Matukio Muhimu ya Binadamu na Takwimu (CRVS) ambao unalenga kuimarisha shughuli za usajili wa matukio muhimu na upatikanaji wa takwimu muhimu kwa maendeleo ya nchi.

Kupitia Mkakati wa CRVS Wizara imedhamiria kukuza na kuendeleza matumizi ya TEHAMA katika usajili wa vizazi na vifo ambapo tayari imezindua mfumo wa kielektroniki wa usajili wa vizazi na vifo kwa kuzingatia mahitaji ambao ulianza kufanya kazi rasmi mwezi Novemba, 2017.

Akiwasilisha Hotuba ya Makadirio ya Bajeti ya Mapato na Matumizi kwa mwaka 2018/19, Waziri wa Katiba na Sheria, Prof. Palamagamba Kabudi anasema katika kipindi cha mwaka 2017/18, jumla ya vizazi 1,593,313, vifo 46,914, ndoa 15,866, talaka 91 na hati 44 za watoto wa kuasili zilisajiliwa nchini.

Anaongeza kuwa Kupitia mradi huo wananchi wanapata huduma za usajili wa vizazi na vifo kupitia ofisi za kata, vituo vya afya na hospitali, ambazo kwa kawaida zipo karibu na wananchi walio wengi, na vyeti vya kuzaliwa na kifo vinatolewa papo hapo.

“Hii ni ongezeko la usajili wa vizazi 201,110, vifo 9,038, hati za watoto wa kuasili 10 na talaka 69 ikilinganishwa na matukio yaliyosajiliwa katika kipindi kama hicho kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 isipokuwa ndoa ambayo ni pungufu ya ndoa 1,907” anasema Prof. Kabudi.

Kwa mujibu wa Prof. Kabudi anasema jumla ya vizazi 929,938 vilisajiliwa na kupatiwa vyeti vya kuzaliwa kupitia Mpango wa Usajili wa Watoto walio Chini ya Miaka Mitano na kufanya kiwango hicho kwa Tanzania Bara kuongezeka kutoka asilimia 13 mwaka 2012 hadi kufikia asilimia 28 mwaka 2017 sawa na ongezeko la vizazi 2,673,806.

Prof. Kabudi anasema Ongezeko la usajili wa matukio ya vizazi na vifo ni kielelezo kuwa RITA imejiimarisha katika kusajili matukio muhimu ya binadamu na kuwataka wananchi kutoa taarifa za matukio hayo katika mamlaka mbalimbali.

Akifafanua zaidi Prof. Kabu vizazi 63,550 vimesajiliwa na kupatiwa vyeti vya kuzaliwa kupitia Mpango wa usajili wa watoto walio shuleni katika Mkoa wa Njombe.

Prof. Kabudi anasema kupitia mfumo huo RITA itaweza kubadilishana taarifa na mifumo mingine ya usajili kama Ofisi ya Taifa ya Takwimu, Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa, Tume ya Taifa ya Uchaguzi na Idara ya Uhamiaji kwa ajili ya kuziwezesha taasisi hizo kufanya maamuzi sahihi, kwa wakati na kwa gharama nafuu.

Anasema kuwa kufuatia taarifa ya utafiti ya mfumo wa Sheria ya Usajili wa Matukio Muhimu ya Binadamu iliyoandaliwa na Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania kwa kushirikiana na RITA, Wizara yake inatarajia kuwasilisha Bungeni Muswada wa Sheria ya Usajili wa Matukio Muhimu ya Binadamu ili kuwezesha matukio mengi zaidi kusajiliwa.

“Wizara, kupitia Wakala wa Usajili, Ufilisi na Udhamini (RITA) pamoja na Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania, imefanya maandalizi ya awali ya kufanyia utafiti mfumo wa kisheria wa ufilisi nchini ili kuweka msingi wa kutungwa upya kwa mfumo wa kisheria wa kuweka mazingira wezeshi ya kufanya biashara na uwekezaji nchini” anasema Prof Kabudi.

Ili mfumo wa CRVS uweze kuleta matokeo yaliyokusudiwa, ni wajibu wa taasisi za umma kuimarisha na kuwa mfumo mmoja wa wa taarifa na mawasiliano katika utambuzi wa matukio mbalimbali ili kuhakikisha kuwa  matukio yanaleta manufaa kwa wananchi na Taifa katika kupanga na kutekeleza mipango mbalimbali ya maendeleo.
Share:

No comments:

Post a Comment

IDADI YA WASOMAJI

TUSIKILIZE LIVE KUPITIA TUNEIN

UNGANA NASI FACEBOOK HAPA

10 ZILIZOSOMWA ZAIDI

Labels

Blog Archive