Waziri Mkuu: Mradi Wa Stiegler’s Utasadia Kutunza Mazingira

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema uamuzi wa Serikali ya awamu ya tano wa kujenga mradi wa kuzalisha umeme kwenye maporomoko ya mto Rufiji, Stiegler’s Gorge utasaidia sana kudhibiti uharibifu wa mazingira nchini.

Akizungumza baada ya kutembelea eneo utakapojengwa mradi huo, leo (Alhamisi, Oktoba 4, 2018), Waziri Mkuu amesema umeme utakaotokana na maji, utazalishwa kwa gharama nafuu na utakuwa wa uhakika zaidi.

Amesema kwa vile umeme utakaozalishwa katika mradi wa Stiegler’s Gorge utakuwa wa bei nafuu na hivyo kuwa rafiki kwa wananchi wa kipato cha chini, utatumika kama nishati mbadala kwa kuni na mkaa  ambao umechangia sana kwenye uharibifu wa mazingira hasa ukataji miti.

Waziri Mkuu Majaliwa amewaomba viongozi wa Serikali na vyama vya siasa wawaelimishe Watanzania kuwa mradi wa Stiegler’s Gorge una faida kubwa kwa Taifa kiuchumi na hauna athari za mazingira na badala yake utayaboresha.

Amewahakikishia Watanzania kuwa mradi huo utajengwa na utakamilika katika muda uliokusudiwa ambao ni miezi 36 kuanzia siku mkandarasi atakapokabidhiwa kazi hiyo.

Akizungumzia usalama katika eneo la mradi, Waziri Mkuu amesema viongozi wa mikoa ya Morogoro na Pwani wahakikishe kwamba wanaweka ulinzi wa kutosha kuanzia sasa na wakati  ujenzi utakapoanza ili kuzuia hujuma  na vitendo vya wizi na udokozi vinavyoweza kuvuruga kasi ya ujenzi wa mradi.

Amesema vifaa vitakavyoletwa na mkadarasi lazima vilindwe na wajenzi watakaoshiriki katika ujenzi wa mradi wahakikishiwe usalama wao na mali zao.

Amewataka wananchi pia washiriki katika ulinzi kwa kutoa taarifa  kwa vyombo vya dola kuhusu watu wenye mienendo inayoweza kuzorotesha ujenzi wa mradi huo kwani jukumu la ulinzi si la polisi peke yao.

Kuhusu ajira kwa vijana wanaotoka katika maeneo yanayozunguka mradi, Waziri Mkuu amesema utaratibu utawekwa ili vijana wenye sifa wapewe nafasi ya kushiriki kwenye usaili na ikibidi watafanyiwa mchujo kwenye maeneo yatakayofikiwa na wengi.

Aliwaasa wote watakaobahatika kupata ajira ya kushiriki katika ujenzi wa mradi huo wawe waadilifu na wachapakazi ili kulinda heshima ya vijana wa Kitanzania na kuwashawishi wajenzi wa mradi kuajiri vijana wengine zaidi.

Kuhusu Wizara ambazo zinaguswa na maandalizi ya ujenzi wa miundombinu inayohitajika katika ujenzi wa mradi wa Stiegler’s Gorge, Waziri Mkuu ameagiza wizara hizo zishirikiane ili kuhakikisha kwamba kila Wizara inatimiza majukumu iliyopangiwa kwa wakati.

Wizara ambazo tayari zimeanza kuweka miundombinu wezeshi kwa mradi huo ni pamoja na Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano inayosimamia ujenzi wa barabara na tawi la reli itakayounganisha eneo la mradi na stesheni ya  Fuga katika reli ya TAZARA kazi ambayo imeanza na Waziri Mkuu wenyewe aliikagua.

Wizara ya maji nayo tayari imetimiza jukumu lake la kupeka maji katika eneo la mradi wakati wizara ya nishati imepeleka umeme. Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi pamoja na Wizara ya Kilimo nazo zipo kwenye eneo la mradi kutimiza majukumu yote yanayozigusa.

Awali, Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani aliishukuru Serikali kwa kukubali kutoa fedha ambazo zimesaidia sana katika ujenzi wa miundombinu ya maandalizi ya ujenzi wa mradi.

IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,
ALHAMISI, OKTOBA 04, 2018.
Share:

No comments:

Post a Comment

IDADI YA WASOMAJI

TUSIKILIZE LIVE KUPITIA TUNEIN

UNGANA NASI FACEBOOK HAPA

10 ZILIZOSOMWA ZAIDI

Labels

Blog Archive