WAZIRI
 MKUU Kassim Majaliwa amesema uamuzi wa Serikali ya awamu ya tano wa 
kujenga mradi wa kuzalisha umeme kwenye maporomoko ya mto Rufiji, 
Stiegler’s Gorge utasaidia sana kudhibiti uharibifu wa mazingira nchini.
Akizungumza
 baada ya kutembelea eneo utakapojengwa mradi huo, leo (Alhamisi, Oktoba
 4, 2018), Waziri Mkuu amesema umeme utakaotokana na maji, utazalishwa 
kwa gharama nafuu na utakuwa wa uhakika zaidi.
Amesema
 kwa vile umeme utakaozalishwa katika mradi wa Stiegler’s Gorge utakuwa 
wa bei nafuu na hivyo kuwa rafiki kwa wananchi wa kipato cha chini, 
utatumika kama nishati mbadala kwa kuni na mkaa  ambao umechangia sana 
kwenye uharibifu wa mazingira hasa ukataji miti.
Waziri
 Mkuu Majaliwa amewaomba viongozi wa Serikali na vyama vya siasa 
wawaelimishe Watanzania kuwa mradi wa Stiegler’s Gorge una faida kubwa 
kwa Taifa kiuchumi na hauna athari za mazingira na badala yake 
utayaboresha.
Amewahakikishia
 Watanzania kuwa mradi huo utajengwa na utakamilika katika muda 
uliokusudiwa ambao ni miezi 36 kuanzia siku mkandarasi atakapokabidhiwa 
kazi hiyo.
Akizungumzia
 usalama katika eneo la mradi, Waziri Mkuu amesema viongozi wa mikoa ya 
Morogoro na Pwani wahakikishe kwamba wanaweka ulinzi wa kutosha kuanzia 
sasa na wakati  ujenzi utakapoanza ili kuzuia hujuma  na vitendo vya 
wizi na udokozi vinavyoweza kuvuruga kasi ya ujenzi wa mradi.
Amesema
 vifaa vitakavyoletwa na mkadarasi lazima vilindwe na wajenzi 
watakaoshiriki katika ujenzi wa mradi wahakikishiwe usalama wao na mali 
zao.
Amewataka
 wananchi pia washiriki katika ulinzi kwa kutoa taarifa  kwa vyombo vya 
dola kuhusu watu wenye mienendo inayoweza kuzorotesha ujenzi wa mradi 
huo kwani jukumu la ulinzi si la polisi peke yao.
Kuhusu
 ajira kwa vijana wanaotoka katika maeneo yanayozunguka mradi, Waziri 
Mkuu amesema utaratibu utawekwa ili vijana wenye sifa wapewe nafasi ya 
kushiriki kwenye usaili na ikibidi watafanyiwa mchujo kwenye maeneo 
yatakayofikiwa na wengi. 
Aliwaasa
 wote watakaobahatika kupata ajira ya kushiriki katika ujenzi wa mradi 
huo wawe waadilifu na wachapakazi ili kulinda heshima ya vijana wa 
Kitanzania na kuwashawishi wajenzi wa mradi kuajiri vijana wengine 
zaidi.
Kuhusu
 Wizara ambazo zinaguswa na maandalizi ya ujenzi wa miundombinu 
inayohitajika katika ujenzi wa mradi wa Stiegler’s Gorge, Waziri Mkuu 
ameagiza wizara hizo zishirikiane ili kuhakikisha kwamba kila Wizara 
inatimiza majukumu iliyopangiwa kwa wakati.
Wizara
 ambazo tayari zimeanza kuweka miundombinu wezeshi kwa mradi huo ni 
pamoja na Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano inayosimamia ujenzi 
wa barabara na tawi la reli itakayounganisha eneo la mradi na stesheni 
ya  Fuga katika reli ya TAZARA kazi ambayo imeanza na Waziri Mkuu 
wenyewe aliikagua.
Wizara
 ya maji nayo tayari imetimiza jukumu lake la kupeka maji katika eneo la
 mradi wakati wizara ya nishati imepeleka umeme. Wizara ya Ardhi, Nyumba
 na Maendeleo ya Makazi pamoja na Wizara ya Kilimo nazo zipo kwenye eneo
 la mradi kutimiza majukumu yote yanayozigusa.
Awali,
 Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani aliishukuru Serikali kwa 
kukubali kutoa fedha ambazo zimesaidia sana katika ujenzi wa miundombinu
 ya maandalizi ya ujenzi wa mradi.
IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,
ALHAMISI, OKTOBA 04, 2018.






No comments:
Post a Comment