Simba Mmoja Awajeruhi Morani 8

Vijana wanane wa jamii ya wafugaji ya Kimasai (morani) kutoka Kitongoji cha Oldonyo Lengai, Kijiji cha Loondolwo, Longido mkoani Arusha, wamenusurika kifo baada ya kujeruhiwa na simba.

Kwa mujibu wa vijana hao, walikutwa na simba majira ya saa nane alasiri juzi kisha kushambuliwa wakati wakichimba kisima kutafuta maji ya kunyweshea mifugo.

"Tulijaribu kupiga kelele, simba akaanza kutushambulia. Kuona hivyo, wengine wakawa wanapiga simu kuomba msaada na kila aliyekuwa anakuja kutoa msaada alishambuliwa," alisema Mibaku Mundesyo (35) mmoja wa manusura hao.

Alisema walishambuliwa maeneo mbalimbali ya mwili hali iliyosababisha moja wao kuwahishwa Hospitali ya Rufani ya Seliani ya jijini hapa kwa matibabu zaidi.

Wengine walionusurika ni Melubo Sung'are (24) Milya Lemayaka (28), Loning'o Sung'are (20), Sakaya Osikarari (20), Ng'ahari ole Bainu (30), Leng'arwua Loda (20) na Laari Olchuda (21).

Kwa mujibu wa jamii ya wafugaji ya Kimaasai, morani wana umri wa miaka kuanzia 18 hadi 40.

Mtaalamu wa wanyamapori na uwindaji anayemiliki kampuni ya uwindaji ya Mantheakis Safaris Ltd, Michel Mantheakis, alisema alimfuatilia simba huyo kuchunguza tukio la kujeruhiwa kwa vijana hao, akabaini kwamba simba ndiye aliyewashambulia vijana hao.

"Ni kweli simba aliwavamia vijana hao lakini jambo la kushangaza hakuweza kuua mtu zaidi ya kuwajeruhi kwa kucha.

"Nilipomfuatilia huyo simba, hakuonekana kuwa na jeraha kwani hata tembea yake haikuwa na shida na kama alirushiwa mkuki haukumpata vyema.

"Nimeshangazwa na tukio hili kwani haijawahi kutokea watu wanane kujeruhiwa na simba bila kuwa kwenye uwindaji,” alisema.

Hata hivyo, aliitaka jamii hiyo wakimwona simba wamwache ili sheria zifuatwe.

Mkuu wa Wilaya ya Longido, Frank Mwaisumbe, aliyefika katika kitongoji hicho na kukutana na wananchi, aliwasihi kuacha kuwinda wanyama kinyume cha sheria.

Alisema wanyamapori huingiza fedha nyingi kijiji hapo kutoka kwa kampuni za uwindaji.

Pia aliwataka kuwa walinzi wa wanyamapori na akalaani vitendo vya baadhi yao kuharibu mitego na kamera zilizowekwa na wawekezaji walioingia nao mikataba.
Share:

No comments:

Post a Comment

IDADI YA WASOMAJI

TUSIKILIZE LIVE KUPITIA TUNEIN

UNGANA NASI FACEBOOK HAPA

10 ZILIZOSOMWA ZAIDI

Labels

Blog Archive