Serikali
 imepiga marufuku Watumishi wa Umma waliohamia Makao Makuu ya Nchi 
Dodoma kwa gharama za Serikali kuomba uhamisho wa kurejea jijini Dar es 
Salaam.
Hayo
 yamesemwa jana na Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi 
wa Umma, Dkt. Laurean Ndumbaro alipokuwa akifanya mahojiano maalum na 
Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) kuhusiana na zoezi zima la uhamisho
 wa watumishi wa umma kutoka Dar es Salaam kwenda Dodoma.
Dkt.
 Ndumbaro amesema kuwa,  Ofisi yake imekuwa ikipokea barua mbili au tatu
 kwa siku za watumishi waliohamia Dodoma kuomba uhamisho wa kurejea Dar 
es Salaam kutokana na sababu mbalimbali ikiwa ni pamoja na za kiafya 
wakati hospitali ya Rufaa ya Benjamin Mkapa ina vifaa vya kisasa na 
uwezo mkubwa wa kutoa huduma za matibabu kwa watumishi hao.
Dkt.
 Ndumbaro amefafanua kwamba,  kabla ya watumishi kuhamia Dodoma, 
Serikali ilitoa maelekezo kwa waajiri kuwasilisha orodha ya watumishi 
wenye matatizo ya kimsingi ili wabaki kwenye vituo vya kazi vilivyopo 
Dar es Salaam wakiendelea kutekeleza majukumu yao.
Dkt.
 Ndumbaro ameongeza kuwa, baadhi ya watumishi waliohamia Dodoma, 
wamegeuza uhamisho huo kuwa mradi  wa kuwaingizia kipato kwani mara 
baada ya kuripoti Dodoma, ndani ya kipindi kifupi wanaomba uhamisho wa 
kurejea Dar es Salaam.
Dkt.
 Ndumbaro amesisitiza kuwa, kutokana na suala hilo, Serikali imetoa 
Waraka wa Barua wenye Kumb. Na. CAC 228/257/01/A/53 wa tarehe 25 
Septemba, 2018 kuhusu Uhamisho wa Watumishi Waliohamia Dodoma Kutekeleza
 Uamuzi wa Serikali Kuhamishia Makao Makuu ya Nchi Dodoma ambao unazuia 
mtumishi aliyehamishiwa Dodoma kwa gharama za Serikali kuomba uhamisho 
wa kurejea Dar es Salaam mpaka atimize miaka mitatu katika kituo cha 
Dodoma.
Watumishi
 wa Umma kuhamia Dodoma ni utekelezaji wa agizo la Serikali lililotolewa
 na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe 
Magufuli tarehe 25 Julai, 2016 wakati wa maadhimisho ya Kumbukumbu ya 
Siku ya Mashujaa.






No comments:
Post a Comment