WAZIRI
 wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kangi Lugola, amefanya ziara ya kushtukiza 
kituo cha Polisi Tabata na Buguruni vya jijini Dar es Salaam ili kujua 
kama maagizo yake aliyoyatoa katika vituo mbalimbali kama yameanza 
kufanyiwa kazi.
Waziri Lugola alianza ziara yake saa 2:45 jana asubuhi kwa kuibukia katika kituo cha Tabata na moja kwa moja alianza kuulizia mahudhurio ya wafanyakazi wote wa kituo hicho na kujua nani yupo kazini na nani hayupo na kwanini hajafika ofisini hapo kwa muda huo wa asubuhi.
Wakati
 alipokua kituoni hapo, pia Lugola alikichukua kitabu cha taarifa za 
watuhumiwa wote waliopo mahabusu na baadaye kuelekea katika mahabusu 
hiyo akiwahoji watuhumiwa kwa kuwaita kwa majina kujua makosa yao 
yaliyoyafanya wawepo kituoni hapo.
Lugola
 baada ya kumaliza katika kituo hicho, saa 5:27 alielekea kimyakimya 
katika kituo cha Polisi cha Buguruni, na aliwahoji watuhumiwa waliopo 
mahabusu katika kituo hicho na kujua makosa mbalimbali yanayowakabili 
huku polisi wapepelezi wa tuhuma zao wakiwepo katika tukio hilo.
Akizungumza
 mara baada ya kumaliza ziara yake, Lugola alisema, alitoa maagizo 
mbalimbali katika ziara zake nchini, hivyo anafuatilia kujua maagizo 
yake yameanza kufanyiwa kazi au bado baadhi ya vituo kama wameyapuuza.
“Lengo
 la hii ziara yangu ni kuboresha utendaji kazi wa vituo vya polisi 
nchini, sijaja kumuadhibu mtu mimi, hivyo msiwe na wasiwasi, bali 
kilichonifanya hapa nije nikufuatilia maagizo mbalimbali ambayo 
niliyatoa kama kweli mnayafanyia kazi,” alisema Lugola.
Maagizo
 aliyoyatoa mwezi miwili iliyopita katika ziara zake mikoa mbalimbali 
nchini ni kuhakikisha pikipiki zinaondolewa katika vituo vya polisi, 
dhamana zitolewe saa 24 ikiwemo Jumamosi na Jumapili, pamoja na polisi 
kutowabambikizia kesi wananchi.
Hata
 hivyo, Lugola alivipongeza vituo hivyo vya polisi vilivyopo wilayani 
Ilala na pia Kituo Kikuu cha Polisi Dodoma alichokitembelea wiki 
iliyopita, kwa kuanza kuyafanyia kazi maagizo yake aliyoyatoa zikiwemo 
baadhi ya bodaboda, zimeondolewa vituoni na zilizobaki zina kesi 
mahakamani.
“Nilifanya
 ziara ya kushtukiza pale Kituo cha Polisi cha Tabata, na pia nimekuja 
hapa Buguruni, kwakweli wameaanza kuyafanyia kazi maagizo yangu, 
pikipiki zote nilizozikuta zinasababu yakuwepo hapo, na si vinginevyo 
kama walivyokua wanaziweka kiholela hapo awali,” alisema Lugola.
Pia
 lugola aliwataka Makamanda wa polisi nchini kuwafuatilia askari wao kwa
 umakini ili kujua utendaji kazi wao, na pia Waziri huyo alisema atakua 
anafanya ziara kama hizo mara kwa mara hivyo vituo vya polisi nchini 
viwe sawa muda wote.
“Hamjui
 siku wala saa ambapo nitakuja, tufanye kazi, tuwahudumie wananchi, 
tusiwaonee wananchi, tujitume kufanya kazi kwa weledi, sitamvumilia mtu 
ambaye atavunja utaratibu,” alisema Lugola.
 






No comments:
Post a Comment