Sakata la Mauaji ya Wananchi Kigoma Linalodaiwa Kufanywa na Wakala wa Misitu Tanzania (TFS) Laibuka Bungeni

Sakata la vifo vya wananchi na polisi mkoani Kigoma vilivyosababishwa na mgogoro wa ardhi hivi karibuni limeibukia bungeni, ikiwa ni siku chache baada ya Mbunge wa Kigoma Mjini (ACT-Wazalendo), Zitto Kabwe kukamatwa na kisha kushtakiwa.

Zitto alikamatwa wiki iliyopita na kushtakiwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam, baada ya mkutano wake na wanahabari kuzungumzia suala hilo.

Wiki chache zilizopita, polisi walikiri kutokea kwa mapigano yaliyosababisha vifo vya watu wawili na askari wawili waliokwenda kwa ajili ya kulinda amani huko Uvinza.

Jana, mbunge wa Viti Maalumu (CCM), Josephine Genzabuke ndiye aliyeliibua bungeni akihoji ni kwa nini Wakala wa Misitu Tanzania (TFS) wamekuwa wakiua na kuwatesa wananchi ambao Rais John Magufuli aliwataka kukaa eneo la Kagerankanda bila ya kuongeza mipaka wakati Serikali ikiwatafutia maeneo mengine.

Baada ya majibu ya Serikali kutoka kwa Naibu Waziri wa Malisili na Utalii, Japhet Hasunga, mbunge Genzabuke alisimama kwa kuuliza swali la nyongeza lililoonekana kumkera Spika Job Ndugai. Genzabuke alihoji,

“Hawa TFS wanaua watu, wanawakata mikono na kuwatesa, kwa nini wanafanya hivyo wakati Rais aliagiza wasibuguziwe.”

Katika swali lake la nyongeza, mbunge huyo alihoji kama TFS wanapingana na agizo la Rais lililotaka wananchi wa maeneo ya Kagerankanda waendelee kulima bila kuongeza maeneo.

Hata hivyo, Spika Ndugai alimzuia kuendelea na swali hilo akisema mambo anayozungumza ni mazito na kumtaka akae chini. Licha ya mbunge huyo kutaka kuendelea kujenga swali lake, lakini aliitwa mbunge mwingine.

Baadaye Ndugai alisimama na kutoa ufafanuzi kwa kukemea maswali aliyosema ni mazito ambayo yalipaswa kupelekwa kwa Waziri Mkuu na si kuulizwa kama ya nyongeza bungeni.

Baada ya kipindi cha maswali na majibu, Mbunge wa Mbozi (Chadema), Pascal Haonga aliomba mwongozo akitaka kuhoji ni kwa nini Spika alimzuia mbunge huyo kuuliza swali la nyongeza.

Spika alimkatiza akisema jambo hilo alishaliondoa kwenye mjadala, hivyo halikuwa na ulazima tena wa kuulizwa mbele ya Bunge.

Awali, katika majibu ya swali la msingi, Naibu Waziri Hasunga alikiri kuwa Rais Magufuli aliagiza ofisi ya mkuu wa Mkoa wa Kigoma kuwapimia wananchi eneo hilo.

Hasunga alisema jumla ya hekta 10,012.61 zilitengwa kwa ajili ya kilimo kwa wananchi wa maeneo hayo na kijiji cha Mvinza kilipewa hekta 2,174, Kagerankanda 2,496 na eneo lingine la hekta 5,342.61 lilitengwa kwa ajili ya wananchi wengine.
Share:

No comments:

Post a Comment

IDADI YA WASOMAJI

TUSIKILIZE LIVE KUPITIA TUNEIN

UNGANA NASI FACEBOOK HAPA

10 ZILIZOSOMWA ZAIDI

Labels

Blog Archive