Sakata
 la vifo vya wananchi na polisi mkoani Kigoma vilivyosababishwa na 
mgogoro wa ardhi hivi karibuni limeibukia bungeni, ikiwa ni siku chache 
baada ya Mbunge wa Kigoma Mjini (ACT-Wazalendo), Zitto Kabwe kukamatwa 
na kisha kushtakiwa.
Zitto
 alikamatwa wiki iliyopita na kushtakiwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi
 Kisutu jijini Dar es Salaam, baada ya mkutano wake na wanahabari 
kuzungumzia suala hilo.
Wiki
 chache zilizopita, polisi walikiri kutokea kwa mapigano yaliyosababisha
 vifo vya watu wawili na askari wawili waliokwenda kwa ajili ya kulinda 
amani huko Uvinza.
Jana,
 mbunge wa Viti Maalumu (CCM), Josephine Genzabuke ndiye aliyeliibua 
bungeni akihoji ni kwa nini Wakala wa Misitu Tanzania (TFS) wamekuwa 
wakiua na kuwatesa wananchi ambao Rais John Magufuli aliwataka kukaa 
eneo la Kagerankanda bila ya kuongeza mipaka wakati Serikali 
ikiwatafutia maeneo mengine.
Baada
 ya majibu ya Serikali kutoka kwa Naibu Waziri wa Malisili na Utalii, 
Japhet Hasunga, mbunge Genzabuke alisimama kwa kuuliza swali la nyongeza
 lililoonekana kumkera Spika Job Ndugai. Genzabuke alihoji,
“Hawa TFS wanaua watu, wanawakata mikono na kuwatesa, kwa nini wanafanya hivyo wakati Rais aliagiza wasibuguziwe.”
Katika
 swali lake la nyongeza, mbunge huyo alihoji kama TFS wanapingana na 
agizo la Rais lililotaka wananchi wa maeneo ya Kagerankanda waendelee 
kulima bila kuongeza maeneo.
Hata
 hivyo, Spika Ndugai alimzuia kuendelea na swali hilo akisema mambo 
anayozungumza ni mazito na kumtaka akae chini. Licha ya mbunge huyo 
kutaka kuendelea kujenga swali lake, lakini aliitwa mbunge mwingine.
Baadaye
 Ndugai alisimama na kutoa ufafanuzi kwa kukemea maswali aliyosema ni 
mazito ambayo yalipaswa kupelekwa kwa Waziri Mkuu na si kuulizwa kama ya
 nyongeza bungeni.
Baada
 ya kipindi cha maswali na majibu, Mbunge wa Mbozi (Chadema), Pascal 
Haonga aliomba mwongozo akitaka kuhoji ni kwa nini Spika alimzuia mbunge
 huyo kuuliza swali la nyongeza.
Spika alimkatiza akisema jambo hilo alishaliondoa kwenye mjadala, hivyo halikuwa na ulazima tena wa kuulizwa mbele ya Bunge.
Awali,
 katika majibu ya swali la msingi, Naibu Waziri Hasunga alikiri kuwa 
Rais Magufuli aliagiza ofisi ya mkuu wa Mkoa wa Kigoma kuwapimia 
wananchi eneo hilo.
Hasunga
 alisema jumla ya hekta 10,012.61 zilitengwa kwa ajili ya kilimo kwa 
wananchi wa maeneo hayo na kijiji cha Mvinza kilipewa hekta 2,174, 
Kagerankanda 2,496 na eneo lingine la hekta 5,342.61 lilitengwa kwa 
ajili ya wananchi wengine.






No comments:
Post a Comment