Baraza 
 la Usimamizi wa Mazingira nchini (NEMC), limekifungia kiwanda cha 
kusindika nyama ya punda kilichopo kwenye Jiji la Dodoma, baada ya 
ukaidi wa muda mrefu wa mmiliki kufuata taratibu sahihi za uhifadhi wa 
mazingira.
Barua
 iliyoandikwa na Kaimu Mkurugenzi wa NEMC, Dk. Vedast Makota,  imeeleza 
kwamba, kiwanda hicho ambacho kinashughulika na uchinjaji na 
usafirishaji wa nyama ya punda nje ya nchi, kwa muda mrefu sasa 
kimeonyesha kushindwa kuzingatia taratibu za uhifadhi wa mazingira, 
licha ya onyo na ukumbusho kadhaa uliofanywa na baraza.
“Kufuatia
 mlolongo huu wa uchafuzi wa mazingira, ambao umekuwa ni kero kwa 
majirani na ambao unaleta mashaka kwenye ubora wa bidhaa, Baraza 
limefikia hatua ambayo linakosa cha kushauri zaidi ya kufunga kiwanda,” 
imeeleza barua hiyo.
Kwenye
 maelezo ya ufungaji wa kiwanda hicho, Dk. Makota alisema: “Kwa mamlaka 
yaliyokabidhiwa kwa Baraza chini ya Kifungu cha 196(2) cha Sheria ya 
Usimamizi wa Mazingira ya mwaka 2004, unaamuriwa kusimamisha shughuli 
zote za uzalishaji kuanzia siku ya agizo hili mpaka utakapochukua hatua 
kikamilifu za kutekeleza maagizo yote uliyopewa hapo awali,” ilieleza 
barua hiyo
Kiwanda
 hicho ambacho kinamilikiwa na kampuni inayofahamika kama Huwachen 
Company Limited, kimekuwa kwenye mvutano wa muda mrefu na Baraza pamoja 
na Wizara inayohusika na uhifadhi wa mazingira tangu Mei, mwaka huu, 
ambapo aliyekuwa Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na 
Mazingira), Kangi Lugola, alitembelea na kueleza kutoridhishwa kwake na 
hali ya uhifadhi wa mazingira.
Ziara
 hiyo ya Naibu Waziri ilitokana na ukaguzi wa NEMC uliofanywa Agosti, 
mwaka huu kwa lengo la kutathmini hali ya uhifadhi wa mazingira kwenye 
kiwanda hicho kutokana na shughuli zake. Katika tathmini hiyo, suala la 
uchafuzi wa mazingira liliendelea kuonekana kuwepo.
Mambo
 yaliyoonekana kuwa ni tatizo ni pamoja na mabaki ya damu kwenye eneo 
hilo ambayo yalipelekea uwepo wa nzi wengi, kuziba kwa mitaro ya 
kupitisha maji machafu, kukosekana kwa utaratibu madhubuti wa kuhifadhi 
mbolea, kiwango duni cha shimo la kuhifadhia uchafu, harufu mbaya na 
ukosekanaji wa mpango endelevu.
Mapungufu
 hayo kwa mujibu wa taarifa hiyo ya Mkurugenzi wa NEMC yanakiuka vifungu
 kadhaa vya sheria ya mazingira ya mwaka 2004, hii ni pamoja na kifungu 
cha 106 (1) (2) na (6) pamoja na kifungu cha 187 (1) (b) na (C).






No comments:
Post a Comment